MAFANIKIO HAYAJI KWA KUOMBEWA ILA KWA MBINU
Watu wengi wamekuwa wakiona mafanikio kama ndoto kwao kwa kuwa wameshindwa
kupata ufahamu sahihi juu ya maisha ya kufanikiwa. Ni kweli watu wengi
wamewekeza jitihada na juhudi nyingi katika kutafuta mafanikio ikiwemo na
kuombewa au kuomba juu ya mafanikio lakini hiyo si misingi wa mafanikio. Leo
nataka ujue misingi ya mafanikio ni mbinu ndio maana shule zikawepo. Watu
wanafikiri tu akiweka juhudi anafanikiwa. Hayo si ya kweli. Juhudi ni jambo
moja linalohitaji mbinu ili izae matunda.
Kila kitu duniani asili yake ni ulimwengu wa roho kuanzia mtu mpaka vitu
anavyotumia kwa kusema hayo kila kitu kina roho ndani yake. Hivyo basi vitu
hivi unahitajika uwe na ufahamu navyo nawe utavitumia utakavyo. Kwa kuwa vyote
asili yake ni rohoni Paulo anatuambia wazi juu ya habari hizi "Vaeni silaha za Mungu mpate kupinga
hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu si juu ya damu na nyama; bali juu
ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya
katika ulimwengu wa roho" Efe 6:11-12. Hivyo basi kama tunataka
kufanikiwa lazima tujifunze mbingu za kiroho za kuvitawala.
Fikiria unafanya biashara na watu wa dini tofauti una uhakika kiasi gani
juu ya njia wanazotumia kufanya biashara? Ili kupata riziki? Kama unataka
kunielewa vizuri nenda kwenye maeneo yenye mfululizo wa vibanda vya chipsi
utagundua licha ya wao kukaa sehemu moja bado mwisho wa siku wanapata vipato
tofauti tena vyenye utofauti mkubwa. Utagundua wazi kwamba hawa jamaa
wanatofautiana mbinu ambazo za msingi ni za ulimwengu wa roho. Ukiwafuatilia
kila kitu wamelingana lakini tofauti yao iko kwenye mbinu za kuvuta wateja
katika ulimwengu wa roho. Kwa kuwa watu ni roho hivyo hutumia mbinu za
ulimwengu wa roho kuwapata. Hujawahi ona mtu anatoa mwanae kafara ili apate
pesa. Hii ni kwa sababu mtu ni roho na anauhusiano na vitu vingine ndio maana
anaweza kutumika kama kivutio cha pesa. Sisemi ufanye hivyo maana hii ni mbinu
ya ufamle wa giza ziko za nuruni na ndizo Bwana anapenda tujifunze leo.
Nataka kukuuliza kufanikiwa kwa nchi ya China kuliletwa na maombi au mbinu
haijalishi ni za madhabahu gani. Tuache kudanganyana kama unapenda kufanikiwa
tafuta namna ya kujifunza mbinu lakini si kila mbinu bali zile za ulimwengu wa
nuru. Watu wengi wanahangaika na maombi bila kuanza na mbinu. Maombi
yanahitajika lakini yana mahali pake. Maombi hutumika kwa ajili ya kutekeleza
mbinu ili zifanikiwe. Sasa watu wengi hutumia maombi bila kuwa na mbinu sijui
wanatekeleza nini? Ndio maana ukiangalia wakristo wengi ni maskini na wasiomjua
Mungu ni matajiri na jambo hili linawasumbua waliokoka kiasi cha kukata tamaa.
Kama utakumbuka mtu mmoja alimwendea Yesu akamuuliza, "Nifanye nini
ili niurithi uzima wa milele?" Huyu mtu alikuwa akitafuta kujua ni mbinu
gani ingemuwezesha kufanikisha safari yake ya kwenda mbinguni kwani alijua
kwenda kanisani haitoshi. Kusoma tu bila kuwa na mbinu za kukusaidia kufaulu
mtihani ni bure maana unaweza kushindwa shule. Hujawahi ona mtu anakuambia mimi
najitahidi kusoma sana lakini sifaulu. Hivi unadhani tofauti ya wa kwanza na wa
mwisho darasani ni nini? Ukijaribu kutazama kwa mapana utagundua ni mbinu.
Jambo la msingi mbinu za mafanikio ni nyingi na hazifanani kwa kila mtu kwa
kuwa hutegemea na mazingira na aina ya mtu. Kila mtu duniani ana mpango wake wa
maisha usiofanana na mtu yeyoye duniani. Hivyo basi kuiga mbinu za mtu huweza
kukukwamisha kimaendeleo. Kwa sababu ya wengi kuwa wavivu wa kusoma biblia na
kufikiri huishia katika kuiga walichofanya wengine wakidhani watafanikiwa. Kuna
msemo, usemao ni mpumbavu tu anayeweza kutumia njia ile ile akiamini itampa
matokeo tofauti.
Mungu ametamani kutupitisha kwenye shule ya namna hii kwa sababu amesema
wazi kuwa mawazo anayotuwazia ni mema kutupa tumaini siku zetu za mwisho. Hivyo
basi ni rai yangu mpendwa unayefuatana nami kwa njia ya Roho Mtakatifu akupe
kuelewa hili ili usikae gizani kamwe maana ndio mpango wa Mungu juu yako.
Barikiwa Na Henry Nicholaus
IJUE SADAKA KWA UNDANI WAKE
Sadaka ni kitu chochote kinachoweza kutolewa na
mtu kama sadaka. Iwe ni kazi za ajira, mashamba, biashara nk. Ili sadaka iwe
sadaka lazima ifanyike kuwa sadaka. Kwa mfano: Noti ya elfu kumi inabaki kuwa
noti ya elfu kumi kabla haijafanyika sadaka. Ili elfu kumi iwe sadaka lazima,
ni lazima iwe sadaka kwa mtoaji, ili ifanyike sadaka kwa mpokeaji. Kinachofanya
elfu kumi iwe sadaka si fedha yenyewe ila ni moyo wa mtu anayeitoa. Kutoka
25:1-2 “Bwana akanena na Musa, akamwambia, waambie wana wa Israeli kwamba
wanitwalie sadaka, kila mtu ambaye moyo wake wampa kupenda mtatwaa kwake sadaka
yangu,” Sasa utanielewa kuwa uhalali wa fedha
kuwa sadaka watoka moyoni na huo humfanya Mungu aipokee.
Kinachofanya gari liwe gari, ni ule mfumo wa utendaji kazi wa injini yake.
Kama vile injini ya ndege ndio inayofanya ndege iwe ndege. Pamoja na kwamba
kuna aina tofauti za magari kama Toyota, Nissan, Ford, Mistubishi nk; bado yote
ni lazima yawe na injini zenye mfumo wa utendaji kazi wa gari kabla hazijawekwa
vitu vinavyoitofautisha aina ya hayo magari. Kumbuka sadaka inafanya kazi kama
gari. Haijalishi anayeendesha ni mchungaji au ni mwizi bado itafanya kazi kama
gari.
Utendaji kazi wa sadaka unafanya kazi kwa kufanana, bila kujali ya kwamba
ni Mungu anayepokea au ni miungu inayopokea. Kwa mfano sadaka inamuunganisha
mtoa sadaka na Mungu aliyepokea au ni miungu iliyopokea. Soma Zab 106:19,28 na
Hes 25:1-3. Pia biblia inatuambia kuwa sadaka inaweza kutumika kumfunga mtu kwa
ajili ya kiapo kwa Mungu aliyeipokea au kwa miungu iliyo ipokea Yos
2:12-13,17-21 na Eze 21:21-23.
Tena biblia inatuambia kuwa sadaka inauwezo wa kutengeneza mahusiano ya
kimaagano, kati ya mtoa sadaka na Mungu aliyeipokea sadaka yake, au na miungu
iliyopokea sadaka yake Zab 50:5. Muunganiko huu haumgusi tu yule aliyetoa
sadaka bali nguvu iliyomo ndani ya sadaka aliyoitoa. Inatoa nafasi na uhalali
wa kugusa watu wengi zaidi yake hata kugusa kizazi zaidi ya kimoja.
Biblia inatupa mifano ya familia kadhaa ambazo hali zake za kimaisha,
kiroho na kimwili zimetengenezwa na utoaji wa sadaka kwa mmoja wa familia zao.
Hebu tazama mfano huu: Ibrahimu aliitoa sadaka hii ya fungu la kumi kwa mara ya
kwanza, kama tusomavyo katika kitabu cha Mwanzo 14:18-20. Sadaka hii si tu
kwamba ilimgusa Ibrahimu na kumwezesha kuwa tajiri bali pia iligusa Lawi na
uzao wake kizazi cha nne.
Maisha yako yaweza yakawa yamejengwa juu ya utoaji sadaka wa uzao wako
uliokutangulia kuzaliwa katika vizazi vilivyopita. Haya tunayaona katika Zab
50:5 ambapo Mungu akasema, "nikusanyieni
wacha Mungu wangu, waliofanya agano nami kwa dhabihu" Hii ni kwa sababu si kwamba
watu walitoa wao lakini walitoa kupitia Ibrahimu ambaye ni baba yao. Hivyo kwa
kutoa kwake sadaka ya agano kuliwagusa mpaka wao.
Kufuatana na Mwanzo 15:13-16 Mungu alimtaarifu Ibrahimu ya kwamba sadaka
yake hiyo, iliyosababisha wakafunga agano pamoja itagusa maisha ya uzao wake
miaka mia nne baadaye! Tunaona jambo hili likitokea katika Kut 2:23-24 wakati
wana wa Israeli wakimlilia Mungu awatoe toka katika kongwa la utumwa huko
Misri. Biblia inasema, "Mungu akasikia kuugua kwao,
Mungu akakumbuka agano lake alilofanya na Ibrahimu.."
Sasa utaona kuwa kuanzia sasa utoaji wako wa sadaka ukibadilika kwa sababu
umepata kozi mpya juu ya sadaka. Hii inatupa sisi kujua ya kuwa bado kuna
hazina kubwa ya maarifa ambayo mimi na wewe twapaswa kuyajua kuwapo duniani ili
kuishi kwetu kuwe na faida kwetu sisi leo, kwa wengine tunaoishi nao na hata
vizazi vijavyo. Lakini yanategemea kama tutajiegemesha katika kufahamu
tunachotakiwa kujua.
Barikiwa Na Henry Nicholaus
JE WAJUA KUWA DHAMBI
HULETA ADHABU, UADUI, UHARIBIFU NA KUFUNGWA KWA MILANGO YA KI-MUNGU KWA
WALIOISHIRIKI
Watu wengi tunatenda dhambi huku tukifikiri tutatubu halafu basi. Leo Mungu
ameleta somo hili kwa watu aina hii ili wajue kutenda dhambi kuna gharama kubwa
kuliko ile tunayofikiri. Na ndio maana kichwa cha somo kinasema, "Dhambi
huleta uadui, adhabu, uharibifu na kufungwa milango ya ki- Mungu kwa
wanaoishiriki". Hii ni somo muhimu sana mpendwa naomba ufuatilie nami ueweze
kuelewa juu ya jambo hili.
Kwanza nataka utambue kuwa tunachambua kilichopo ndani ya 'sheria ya dhambi
na mauti'. Sitaweza kuchambua tena sheria ya dhambi na mauti ni nini, kama
huijui ni vema ukatafuta somo moja wapo katika kurasa hii katika hii blog
liitwalo "KWA NINI TUNAFANYA MAOMBI YA TOBA" .Hapo utaelewa juu ya
sheria ya dhambi na mauti kisha rudi uendelee kusoma somo hili.
"Bwana
akamwambia Musa, Haya! shuka; kwa maana watu wako uliowatoa katika nchi ya
Misri wamejiharibu nafsi za, wamepotoka upesi kuiacha ile njia niliyowaamuru,
wajifanyizia ndama ya kuyeyusha, wakaiabudu na kuitolea dhabihu, wakasema, Hiyo
ndiyo miungu yako, Ee, Israeli, iliyokutoa katika nchi ya Misri. Tena Bwana
akamwambia Musa, Mimi nimewaona watu hawa na tazama ni watu wenye shingo ngumu,
basi niache, ili hasira zangu ziwake juu yao, niwaangamize; nami nitakufanya
wewe uwe taifa kuu." Kut 32:7-10
Anagalia maneno yafuatayo na maana zake kama yalivyotumika katika kifungu
hapo juu cha maandiko. Neno 'Basi niache ili
hasira yangu' hili lilikuwa linaonyesha kuwa Mungu alitaka kuwapa adhabu juu ya dhambi
ya kuabudu miungu waliofanya. Pia neno 'Niwaangamize'
limeonyesha juu ya
uharibifu utakaotokea juu yao. Vilevile neno 'Nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa' inaonyesha kufungwa kwa milango ya ki-Mungu
katika maisha yao.
Na ukisoma Kut 33:2 unaona kuwa Mungu anamwambia Musa licha ya kwamba
amebadili msimamo wa kuangamiza Israeli lakini hataendelea nao katika safari
bali atawapa malaika ambaye atawaongoza katika safari. Hii inamaanisha kuna
kitu kilisababisha 'uadui' kuinuka kati ya watu na Mungu. Na uadui huu
uliinuka kwa sababu ya dhambi. Na pia unaweza kunielewa vizuri kama ukisoma Efe
2:13-16, Paulo ametumia maneno yasemayo damu ya Yesu imetumika kuondoa kiambaza
kwa tafsiri ya kiambaza ni uadui. Kwa hiyo kama angetumia maneno ya kawaida
angesema, Damu ya Yesu ili tumika kuondoa uadui.
Kwa hiyo nimekuonyesha dhambi inaachilia nini pale unapoitenda, angalia kwa
karibu maneno yaliokolezwa wino kama hujanielewa. Kwa dhambi ya kuabudu miungu
Musa alifanya toba 5 za aina tofauti ili kuwasaidia wana wa Israeli warejee
hali yao ya kawaida ya kimwili na kiroho. Hii ina maanisha nini tunaweza kufanya
dhambi halafu ikatuadhiri sana hata kama una elimu juu ya sheria ya dhambi ya
mauti usifanye makusudi jifunze kuzuia kumbuka aina ya toba alizofanya Musa
zilimgharimu muda sana, kwa kuwa sio jambo rahisi.
Nikukumbushe kuwa kujirusha ndani ya shimo ni rahisi kuliko kutoka ndani ya
shimo. Hivyo ni vyema ukaomba Mungu akusaidie uepuke kufanya dhambi. Mungu
anaposema kuwa anakuwazia yalio mema ndio maana yake ni pamoja na kujua ukweli
juu ya mambo mbalimbali kama huu aliokupa leo. Toba ina mambo mengi haya uliojifunza
leo si ukomo kwa kuwa hatufiki ukomo wa kujifunza neno la Mungu duniani
twahitajika kujifunza kila iitwapo leo.
Barikiwa sana
Na
Henry Nicholaus
No comments:
Post a Comment